#Baada ya shule, kama vijana tunafanya jitihada za kutafuta kazi tuwe na maisha mazuri, kwa maneno mengine naweza kusema, tuondokane na umaskini. Katika kupigania hilo tunajikuta tunaendesha maisha fulani ambayo yanatulevya na baadaye tunajikuta hatuna tena nguvu ya kuyabadilisha. Tunaingia katika madeni ili tuweze kuyaendesha maisha hayo ya mapicha picha. Alafu mioyoni tunajidanganya kwamba hayo ni maisha mazuri na yanaonyesha sisi tuna uwezo. Ni kweli kwamba mtu anaweza kuishi maisha ya sinema, ili aonekane na watu kuwa ana hiki na kile wakati kiukweli akijiangalia yeye mwenyewe kwa mapana ni maskini wa kutupwa. Unaweza kuwa na kazi yenye mshahara mkubwa na huo mwenendo wako wa maisha ukakudanganya kwamba unaelekea pazuri lakini kiukweli ikawa ni kinyume kabisa.
#Utajuaje kama sasa huku ninakoelekea nitakua maskini? Angalia hizi dalili na kama utakua uko katika kipindi cha mwanzo cha kuajiriwa ikusaidie ili usijikute kwenye mashimo yaliyowachota wengi.
#Kwanza, huwezi kuishi bila Mshahara wako, kiasi kwamba mshahara ukicheleweshwa wiki moja tu unaandamana mitaani, au mishahara ya miezi miwili haikutani. Wote wanaanza kama hivi, tunahitaji mishahara kulipa kodi, kununua chakula, kulipa ada za watoto, na nyingine tuweze ku-enjoy kidogo, hakuna anayebisha katika hili, lakini unashauriwa hili lisiwe la muda mrefu, unapoanza kazi jitahidi ifikie muda ili uweze kuishi bila kutegemea mshahara wako.
#Isiwe mshahara ukicheleweshwa basi wewe ni kulia njaa tu. Kulifanikisha hilo inamaana kipande cha mshahara wako inabidi ukihifadhi, na kadri unavyokua ndo kipande hicho unachokata kwa ajili ya kuhifadhi kiongezeke na chenyewe. Na vile vile uweze kuwekeza. Stori za wewe kuhamia kwenye jumba kubwa, kwenda baa za bei ghali, magari makubwa waachie Bongo movies, wao ndo wana haki ya kuigiza hata maisha hayo maana kazi yao kubwa ni uigizaji. Hayo yote kwako yanakufanya tu uendelee kutegemea mshahara wako.
#Sababu nyingine ni kumiliki vitu vingi vyenye thamani ya pesa lakini visivyodumu. Kuwa na gari zaidi ya moja tena ya bei mbaya, TV imeziba ukuta mzima na mengineyo, na gharama ya hivyo vyote vinazidi kile ulichokiwekeza kwenye hisa, biashara au vitu vingine vyenye thamani isiyopungua kama Ardhi. Ikiwa hivi rafiki yangu nakushauri ufanye kinyume, ikiwezekana uza kabisa hiyo TV ukanunue Hisa TBL au TCC. Gari ulilonunua leo milioni 30, mwakani huwezi kuliuza kwa milioni 30, na hata kama utauza milioni 30, uwezo wa milioni 30 hiyo hautakua ni ule wa mwaka jana.
#Fanya uamuzi kwa makini au Maamuzi magumu, wekeza pesa zako sehemu au kwenye vitu visivyopungua thamani. Na kamwe usije uza vitu kama ardhi ili ununue gari, au uende likizo. Ukijikuta unatumbua fedha zako kumfurahisha fulani.
#Tunalazimika kuamini kwamba, simu tunazotumia, nguo tunazovaa, sehemu tunazoishi, magari tunayoendesha au viwanja tunavyoenda kufurahi vinatujengea heshima fulani katika jamii, niamini mimi ‘no body cares’ ukifeli maishani unakua ni wewe na Mungu wako. Hao unaodhani wanakuheshimu kwa unachokifanya hawatakuwepo na si ajabu wakaanza kukukimbia mitaani ukitokeza tu. Alafu ni adhabu, maana kama watu walikuheshimu kisa ulikuwa na Passo cc 1000 sasa inabidi usishuke chini, upande juu kwenye Brevis cc 2000, kumbuka na matumizi ya mafuta yanapanda, unazidi kupunguza kipande chako cha kuwekeza. Huu mzunguko unaendelea mpaka inafika kipindi unaishiwa kabisa.
#Kutumia fedha ulizozipata kwa jasho lako haijawahi kuwa mbaya, tena tunaamini utakapotumia ndo nguvu ya kutafuta nyingine inakuja haraka, ubaya ni pale unapokua na maamuzi mabaya juu ya matumizi yako. Na vile vile unapochukua mkopo ili utumie na wala sio kufanya ule mkopo uzalishe kitu fulani. Hii inamaanisha ulichukua mkopo uendeleze yale maisha yako ya picha picha na wala haukuzalisha chochote. Mwisho wa siku, mikopo ya aina hii inakufanya uanze kutumia zaidi ya kipato chako. Sisemi usikope kabisa, kopa kwa misingi ya kuzalisha kitu, hata mkopo ukirudi unakua na kiasi fulani cha fedha ambacho aidha utakitumia au kukiwekeza kwa manufaa yako.
#La mwisho ninaloweza kuongelea leo ni kuwa na mipango katika maisha yako. Kama utapangilia vizuri maisha yako, umasikini utaishia kuuona kwenye TV na kusikia tu kutoka UN kwamba kuna Watanzania wanaoishi chini ya dola 1.
#Njia unayochukua au kuchagua maishani mwako hakikisha inakupeleka sehemu ambayo ukikaa chini wewe mwenyewe uangalie nilikua huku na sasa niko hapa. Na hakuna mwingine atakaekuja kukuwekea msimamo wa wewe kujitegemea zaidi yako. Na siku zote kwa kuangalia ni mwanzo wala sio mwisho.
#Ukianza na misingi mizuri utafika pazuri. Unatakiwa ufike mahali useme kazi au biashara yangu niliyofanya kuanzia mwaka fulani mpaka mwaka fulani, imenisaidia kufanya hiki na kile. Na ukiwa na mipango yako unayotakiwa kukamilisha, ni lazima utajipimia hata katika matumizi yako ili uweze kufikia malengo yako. Maisha ya mapicha picha tuyaache huko huko Instagram kwa waigizaji.
#Impersonation is good while you round among many but in dispersion is the great regret of your does, take care take care dear Rafiki.
© 2016. All rights reserved @ Sir Lalian Mwittah Nyalali.
No comments:
Post a Comment